NA ESTOM SANGA-MBEYA
Waziri wa
nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mheshimiwa
George Mkuchika amewatembelea Walengwa wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii-TASAF
katika halmashauri ya Jiji la Mbeya na kuwataka kuongeza jitihada zaidi za
kujitegemea kwa kutumia ruzuku wanayoipata kwa kuanzisha miradi ya uzalishaji
mali ili kukuza kipato chao.
Mheshimiwa
Mkuchika amesema jitihada za serikali kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Jamii-TASAF
za kuhamasisha wananchi kuuchukia umasikini haziwezi kuwa endelevu ikiwa
walengwa wa Mpango wa Kunusuru Kaya masikini hawatatumia fedha wanazozipata
kubuni miradi ya uzalishaji mali.
“hiki
mnachokipata kutoka serikalini kupitia TASAF kiwe chachu ya kuanzisha miradi ya
uzalishaji mali ili hatimaye muweze kujitegemea” amesisitiza Waziri Mkuchika.Akiwa katika
eneo la Shule ya Sekondari ya Lupeta katika jiji la Mbeya , shule ambayo TASAF
imejenga jengo la Utawala na Maabara,Waziri Mkuchika ameeleza kuridhishwa na
matokeo ya ujenzi wa majengo hayo na kupunguza kero iliyokuwa inawakabili
walimu na wanafunzi shuleni hapo.
Aidha
Mheshimiwa Mkuchika amekutana na vikundi vya uzalishaji mali vilivyoanzishwa na
Walengwa wa TASAF kwa kutumia ruzuku ya fedha kupitia Mpango wa Kunusuru Kaya
Maskini ambapo walengwa hao wamekuwa wakikopeshana fedha zinazotokana na
uzalishaji wa bidhaa zikiwemo mikeka,na hivyo kuwaongezea uwezo wa kuhudumia
kaya zao.
Hata hivyo
Waziri huyo ametoa maagizo kwa uongozi wa mkoa wa Mbeya kuhakikisha kuwa watu wanaonufaika na
fedha za ruzuku kutoka TASAF ni wale wanaokidhi vigezo vya umasikini na kutaka
fedha zilizolipwa kwa watu wasiostahiki zirejeshwe mara moja.
“rejesheni
fedha za serikali ili ziwanufaishe walengwa wanaostahiki kupata ruzuku hiyo
kama ilivyokusudiwa na serikali” ameonya Waziri Mkuchika.Kwa upande
wake Mwakilishi wa Mkurugenzi Mtendaji wa TASAF,Bi. Mercy Mandawa ameishukuru
serikali kwa kuendelea kuusimamia kikamilifu Mfuko wa Maendeleo ya Jamii TASAF
ili uendelee kusaidia jitihada za kuwaondolea wananchi kero ya umaskini.
Amesema
tangu kuanzishwa kwa Mpango wa Kunusuru Kaya Masikini ,kumekuwa na mwitikio
chanya kwa walengwa kutumia ruzuku hiyo kuboresha maisha yao huku mkazo
ukiwekwa katika kuboresha elimu,afya na lishe kwa watoto wanaotoka kwenye kaya za walengwa huku akisisitiza juu
ya matumizi sahihi ya ruzuku inayotolewa kila baada ya miezi miwili.
Waziri wa
Nchi Ofisi ya Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. George Mkuchika (aliyevaa suti nyeusi)
akikagua bidhaa zilizotengenezwa na Walengwa wa TASAFkatika mtgaa wa Inyala
katika jiji la Mbeya kama njia mojawapo
ya kujiongezea kipato.
Waziri
Mkuchika (aliyevaa tai) akimsikiliza mmoja wa wanafunzi wa shule ya sekondari
ya Lupeta katika jiji la Mbeya alipotoa maelezo ya maabara iliyojengwa na TASAF
shuleni hapo.
Waziri wa nchi ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma
na Utawala Bora Mhe. George Mkuchika akikagua jengo la maabara lililojengwa na
Mfuko wa Maendeleo ya Jamii-TASAF katika shule ya Sekondari ya Lupeta katika
halmashauri ya jiji la Mbeya.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...