Na Nyakongo Manyama-Maelezo
Chama cha Wakulima Tanzania (AFP) kimepongeza hotuba ya Rais wa awamu ya
Tano wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt.John Pombe Magufuli
aliyoisoma wakati wa ufunguzi wa Bunge la 11, Novemba 20 mwaka huu mjini Dodoma.
Akiongea katika mkutano na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam
Mkurugenzi wa Mahusiano wa Makundi Maalum wa AFP Bw. Peter Sarungi
ameeleza kuwa hotuba hiyo imesimama katika mambo ya msingi na yenye kuleta
mabadiliko ya kuijenga Tanzania mpya.
Aidha Sarungi aliongeza kwa kusema anaamini kupitia kauli mbiu ya hapa kazi tu
uchumi wa nchi utakua na kuboresha huduma za afya,upatikanaji wa elimu kwa
watu wote ,kupanda kwa thamani ya shilingi ya Tanzania,kuongeza heshima ya
uchumi nje na ndani ya na kuwa na viongozi wawajibikaji.
“kwa kweli hotuba ya rais imegusa nyanja zote muhimu ikiwemo namna ya
kukabiliana na kuondokana na rushwa,upatikanaji wa vituo vya afya bora,elimu na
mimi naunga mkono jitihada hizi zenye tija ya kuleta mabadiliko ” alisema Sarungi
Sarungi amekemea vitendo vya utovu wa nidhamu vinavyofanywa na baadhi ya
wabunge ikiwemo matumizi mabaya ya lugha za kejeli na kuzomea hali ambayo
inaharibu utendaji wa kazi za Bunge na kuleta mgawanyiko baina yao .
“Kuna umuhimu wa kuziangalia upya kanuni za kudumu za bunge kwa
kuongezwa vifungu vya kuzuia na kutoa adhabu kali kwa mtu yeyote ndani ya
ukumbi wa bunge kutumia maneno ya vijembe, kejeli, misemo ya mafumbo na
lugha za kuudhi ziwekewe msisitizo wa kuzikomesha ikiwemo kutoa adhabu kali
ya kutandikwa viboko” alisema Sarungi.
Mwisho alitoa rai kwa wabunge kuzingatia mambo ya muhimu yaliyowapeleka
bungeni ikiwemo kusimamia na kutetea maslahi ya wananchi na kujenga umoja na
upendo bila kujali itikadi za vyama vyao ili kujenga Tanzania mpya.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...