Mkurugenzi wa Huduma za Kinga Dkt. Neema Rusibamayila toka Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani) mapema hii leo jijini Dar es Salaam kuhusu maadhimisho ya wiki ya unyonyeshaji inayotarajiwa kuanza Agosti Mosi hadi Saba ambapo kitaifa itafanyika mkoani Dodoma.

Na. Eliphace Marwa – Maelezo.

Katika kuzingatia na kuboresha afya ya mtoto, Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii imeendelea kuwahimiza wanawake kuzingatia utunzaji na ustawishaji wa watoto kwa kuwapa haki ya kunyonya maziwa ya mama.

Akizungumza na waandishi wa habari kwa niaba ya katibu Mkuu wa Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, Mkurugenzi wa Huduma za Kinga Dkt. Neema Rusibamayila amesema wakati Tanzania inategemea kuungana na mataifa mengine duniani ni vema jamii ikatambua umuhimu wa lishe kwa mtoto.

“Jamii inapaswa kutambua umuhimu wa unyonyeshaji maziwa ya mama pekee katika miezi sita ya mwanzo ya maisha ya mtoto na kuendelea kunyonyeshwa mpaka umri wa miaka miwili au zaidi” alisema Dkt. Neema.

Kwa upande wa mtoto, Dkt. Neema alisema maziwa hayo yana faida nyingi ikiwemo kumpatia virutubisho vyote anavyohitaji kwa uwiano sahihi kwa afya na ustawi kwani viini vya kingamwili vinavyofanya kazi kama chanjo dhidi ya maradhi humeng’enywa na kufyonzwa kirahisi zaidi mwilini tofauti na vyakula vingine.

Aidha aliongeza kuwa maadhimisho ya mwaka huu yataenda sanjari na kilele cha maadhimisho ya miaka 25 ya Azimio la Innocenti la mwaka 1990ambalo linasisitiza umuhimu wa kulinda, kuendeleza na kusaidia unyonyeshaji na ulishaji bora wa watoto.

Mgeni rasmi katika Maadhimisho hayo yanayotarajiwa kuanza Agosti Mosi na kufikia kilele chake Agosti 7 mkoani Dodoma katika viwanja vya Nanenane ni Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii Dkt. Hussein Mwinyi yakiwa na kauli mbiu “Unyonyeshaji na kazi, hakikisha inawezekana” yenye lengo la kuwasaidia wanawake wote wenye ajira rasmi na zile zisizo rasmi waweze kutunza watoto wao ipasavyo pasipo kuathiri ajira zao zinazowapatia kipato.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...