Afisa Mtendaji Mkuu wa Shirika la Usafiri Dar es Salaam (UDA), Bw John Samangu (kushoto) akikata utepe kuzindua rasmi albamu ya kwanza kutolewa na ya kwaya ya Kanisa la Kigango cha Mtakatifu Rita wa Kashia ijulikanayo kama ‘Msifuni Bwana’ jijini Dar es Salaam hivi karibuni. Wanaoshuhudia ni mwenyekiti wa Kigango cha Mt. Rita Bw. Frederick Msumali(kushoto) na waumini wengine.
Afisa Mtendaji Mkuu wa Shirika la Usafiri Dar es Salaam (UDA), Bw. John Samangu, akionyesha moja ya DVD wakati wa uzinduzi wa albamu ya kwaya ya Kigango cha kanisa la Mtakatifu Rita wa Kashia iitwayo ‘Msifuni Bwana’ jijini Dar es Salaam hivi karibuni. Wanaoshuhudia ni Padre Xavery Kassase, Paroko Msaidizi wa Parokia ya Kanisa Katoliki la Mavurunza (kulia) na Mwenyekiti wa Kigango cha Mt. Rita Bw. Frederick Msumali(kushoto).
Afisa Mtendaji Mkuu wa Shirika la Usafiri Dar es
Salaam (UDA), Bw John Samangu (kulia), akifungua moja ya kanda za albamu ya
‘Msifuni Bwana’ ya kwaya ya Kanisa la Kigango cha Mtakatifu Rita wa Kashia
jijini Dar es Salaam hivi karibuni. Anayeshuhudia ni mwenyekiti wa Kigango cha
Mt. Rita Bw. Frederick Msumali (kushoto).
JAMII imeombwa kusaidia
kuinua muziki wa injili unaofanywa na madhehebu mbalimbali ya dini ya nchini
ili kusaidia kukuza maadili mema miongoni mwa wanajamii.
Akizungumza wakati wa
uzinduzi wa albamu ya kwanza kuwahi kutambulishwa na kwaya ya kigango cha kanisa
la Mtakatifu Rita wa Kashia jijini Dar es Salaam hivi karibuni, Afisa Mtendaji
Mkuu wa Shirika la Usafiri Dar es Salaam (UDA), Bw. John Samangu, ambaye
alikuwa mgeni rasmi katika uzinduzi huo, alisema kuwa albamu hiyo inayobeba
jina la ‘Msifuni Bwana’ itasaidia kukuza maadili mema katika jamii, kwani
nyimbo nyingi katika albamu hiyo zimebeba ujumbe mzuri.
Bw. Samangu alikuwa mtu wa
kwanza kununua nakala tatu za DVD na albamu hiyo ambayo ni ya kwanza kuwahi
kutambulishwa na kwaya ya kigango cha kanisa la Mtakatifu Rita wa Cascia tangu
kuanzishwa kwake mwaka 2010.
Alisema kutokana na hali
iliyopo sasa ya kuporomoka kwa maadili katika jamii, kuna umuhimu mkubwa wa
taasisi kama makanisa kuhimiza watu kubadili tabia zao ili ziwe nzuri na zenye
kupendeza. Alisema muziki wa injili ni miongoni mwa njia za kufikisha ujumbe
utakaokuwa na athari chanya kwa walengwa wengi zaidi.
“Naisihi kwaya ya kigango
cha kanisa la Mtakatifu Rita wa Kashia kuendelea kusambaza neno la Mungu, kwani
kwa kupitia muziki pekee, idadi kubwa ya watu inaweza kufikiwa. Hii itasaidia
jamii kubadilika na kuwa katika mlengo ulio sahihi,” alisema Bw. Samangu.
Kwa upande wake, Paroko
Msaidizi wa Parokia ya kanisa la Mavurunza, Padri Xavery Kassase, alisifu
kitendo cha kwaya hiyo kutafsiri nyimbo zote katika albamu hiyo kwa kutumia
lugha mbalimbali. Alisema kitendo icho kitasaidia albamu hiyo kuwafikia
wasikilizaji wengi zaidi hata nje ya mipaka ya Tanzania.
“Kwa kuzitafsiri nyimbo
kwenye lugha mbalimbali, inamaanisha kuwa mtaweza kusambaza albamu yenu nje ya
nchi na hata kutumia mitandao ya kijamii kama YouTube ili watu wengi zaidi
waweze kusikiliza na kuelewa ujumbe mzuri unaopatikana katika nyimbo hizi.
Naiomba kwaya isiridhike
na mafanikio waliyoyapata hadi kufikia sasa badala yake waendelee kufanya kazi
kwa bidii kuhakikisha kuwa inakuwa miongoni mwa kwaya bora zaidi nchini
Tanzania,” alisema Padri Kassase.
Mbali na hilo, Padri Kassase
aliwaomba watu wauunge mkono muziki wa injili kwani unabeba ujumbe wenye
mafundisho yanayohimiza maadili mema katika jamii badala ya kushabikia nyimbo
zinazoshabikia mambo maovu.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...